1. Nenda kwenye maudhui
  2. Nenda kwenye orodha kuu
  3. Nenda tovuti zaidi za DW

Urusi yatumia kura ya turufu kuikinga Pyongyang

Amina Mjahid
29 Machi 2024

Urusi imetumia kura yake ya turufu kupinga kurefushwa kwa muda wa kundi la wataalamu wa Umoja wa Mataifa wanaofuatilia vikwazo vya kimataifa vilivyowekwa Korea Kaskazini, kufuatia mipango yake ya silaha za nyuklia.

https://p.dw.com/p/4eFZx
Putin
Rais wa Urusi Vladimir Putin Picha: Maxim Shemetov/REUTERS

Hatua hii imejiri wiki kadhaa baada ya kundi hilo la wataalamu kusema linachunguza ripoti ya ubadilishanaji wa silaha kati ya Urusi na Korea Kaskazini. 

Uamuzi wa Urusi umezua hisia mseto. Marekani kupitia msemaji wa wizara ya mambo ya nje Mathew Miller imesema Urusi imetumia Kura ya turufu kwa manufaa yake binafsi na juhudi za kuzuwia kundi hilo kuchunguza maovu yake na Korea Kaskazini.

Korea Kaskazini ilipeleka makontena 7,000 ya silaha Urusi

Nayo Wizara ya masuala ya kigeni ya Korea Kusini imesema Urusi imefanya uamuzi usiofaa licha ya kuwa mwanachama wa kudumu wa Baraza la usalama la Umoja wa Mataifa.